Tuesday, 1 April 2014

IJUE IBADA YA KWELI.



IJUE  IBADA YA KWELI.
Yohana  4:20-24
MWANDISHI:
PASTOR. SONGWA .M. KAZI
GLORY TO GLORY CHRISTIAN CENTRE
TAG –GGCC  FOREST  KONGOWE,
S.L.P. 70983, DSM
SMU: 0757-567-899 /  0789-567-899
Whasap:  0719-968-160
Blog: www.lcm2014. blogspot.com


YALIYOMO:
1.           Maana ya ibada.
2.           Aina  za ibada.
3.            Jinsi ya kumwabudu Mungu katika  roho na kweli. [ method of worship ].
4.           Sura , picha  au mwonekano  wa  ibada  inayo  kubalika.
5.           Sifa za jumla za mwabudu .
  6.     Ibada isiyo kubalika mbele za Mungu.
 7.     Tofauti kati ya Huduma na Ibada



SHUKURANI
·      Kipekee kabisa na mshukuru sana Mungu wangu BWANA Yesu Kristo aliye niita kwa wito mtakatifu kwa kuniokoa na kunitenga kwa ajili ya utumishi katika ufalme wake.

·      Pili; namshukuru Yesu wangu kwa kunipa mke mwenye busara Miriam Songwa Kazi na wanangu Meshach, Prince na Amani kwa maombi na uvumulivu wao kwangu pindi walipo nikosa nikiwa katika maandalizi ya kazi hii njema unayo isoma sasa.

·      Tatu; ninazo shukurani zangu nyingi kwa baba na rafiki; Mchungaji wangu kiongozi Askofu Victor  A.  Tawete na familia yake kwa ushauri , kunitia moyo, kuniombea na kwa mafundisho yake yaliyo kuwa na mchango mkubwa kwenye maandalizi ya kitabu hiki.

·      Nne; nina washukuru kipee wazazi wangu, rafiki zangu kipenzi na watenda kazi pamoja nami katika kazi ya Injili ya ufalme wa Mungu; wana Life Changing Ministry International [ LCM ] na wachungaji wote rafiki zangu kwa maombi yao na ushauri wao. Mungu awabariki sana.

WASIFU WA MWANDISHI  NA KITABU:

o  Mchungaji Songwa M. Kazi , ni mtumishi wa Mungu ambaye amekuwa akifanya huduma za Mikutano ya Injili, Semina, Ushauri na Maombezi  kwa watu wengi ndani na nje ya nchi ya Tanzania kwa zaidi ya miaka 15 sasa. Ni mtenda kazi makini wa Injili ya Kristo mwenye maono ya kuleta matengenezo, uamsho na urejesho katika mwili wa Kristo ulimwenguni bila kuwa na mipaka ya udhehebu.

Kwa sasa ni Mchungaji Msaidizi katika kanisa la GLORY  TO  GLORY  CHRISTIAN  CENTRE  [ TAG- GGCC   FOREST KONGOWE, DSM ];  Pia  ni mkurugenzi wa  Huduma iitwayo Life Changing Ministry International [ LCM ] yenye makao yake makuu Dar -es -Salaam .

o  Kuhusu Elimu,  anayo elimu ya Biblia  kutoka AFRICAN LEADERSHIP INTERNATIONAL [ AL ] ngazi ya cheti na kwa sasa anachukua masomo ya Shahada ya Kwanza katika Huduma, Utawala na Uongozi katika  chuo cha T-NET INTERNATIONAL.

o  Mbali na Huduma hizo, ni  mwandishi wa vitabu vya kiroho vyenye mafundisho shadidi katika ulimwengu wa sasa. Katika kitabu chake cha “ IJUE IBADA YA KWELI” , Mchungaji. S. Kazi ,  kwa kweli ameweka mwongozo muhimu wa namna mwamini anavyoweza kuuridhisha moyo wa Mungu kwa ibada ya kweli tena ya rohoni. Hivyo ukiwa na IJUE IBADA YA KWELI, utakuwa umejiweka kwenye nafasi sahihi ya kutoa manukato safi na mazuri mbele za BWANA wakati wa ibada, yaani kutoka chini ; kwetu  sisi  kwenda juu  kwa BABA ambako hutoka rehema, neema na Baraka.


o  Mchungaji Songwa Kazi ana mke na watoto watatu wa kiume.

§  Na; Ev. Abraham JC. Magoma, Mwanatheolojia wa karne ya 21 , mwalimu wa chuo cha Biblia na Katibu Mkuu wa huduma ya Life Changing Ministry International [ LCM ].








UTANGULIZI:
Je, umewahi kujiuliza kwa nini unakwenda kanisani?
Najua wengi watajibu kuwa , wanakuja au wanakwenda kanisani kuabudu; kitu ambacho ni kweli kabisa. Ila cha ajabu leo,  asilimia kubwa ya waamini hao hawaji kanisani kwa lengo hilo, bali wengi wao wanakuja kanisani kwa lengo la kupokea tu; yaani hawapo kiibada bali wapo kihuduma zaidi. [ they are not after worship but they are ministerial minded / they are after receiving .] Pia wengine  hudhani kuwa kuabudu ni kuimba nyimbo fulani za polepole kwa sauti ya upole na kusifu ni kule kuimba nyimbo fulani za harakaharaka. Kitu ambacho siyo kweli hata kidogo!
Kumbuka kuwa, nyimbo, muziki na mahubiri siyo ibada ; bali ni funguo tu za kutupeleka kwenye ibada. Ibada si jambo la mara moja au kipindi fulani maalumu; bali ibada ndiyo aina au mtindo wa maisha ya kila siku ya  mwamini. Jumla ya maisha yako ndiyo ibada yako; yaani kile kinacho chukua nafasi kubwa katika muda wako, pesa zako, mazungumzo yako , moyo wako, akili zako na nguvu zako


SURA YA KWANZA:
MAANA YA IBADA.

o  Ibada  ni heshima [ respect ] inayotolewa na mtu kwa bwana wake kwa lengo la kumfanya ajisikie tu  vizuri. Elewa wazi kuwa neno  ibada halimanishi kuwa ni takatifu bali kile unachokiabudu ndicho kitakacho amua na kutueleza aina yako ya  ibada.

Ibada  ni kitendo cha kuanguka chini ya miguu ya  bwana wako na kuibusu miguu yake au mikono; tendo amabalo Wagiriki  [ wayunani ] huliita ; proskuneo . Katika mazingira haya;  tunaweza kusema kwamba:
Ibada ni utii [obedience] – yaani kufanya au kutekeleza jambo ulilo agizwa bila kuhoji.
Ibada ni sadaka inayotolewa kwa Mungu.

Heri kutoa kuliko kupokea; Matendo 20:35b
Ibada ikiwa kama sadaka hulenga maeneo makuu matatu  ya kutoa; ambayo ni:-

i. Kujitoa mwenyewe [ giving your self ]:
“Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana.”  Warumi 12:1

ii. Kutoa Mambo Ya Ujazayo Moyo [ Heart  Attitudes ]:
“Na huyo mwanamke alikuwa na uchungu rohoni mwake , akamwomba BWANA  akalia sana.
Hana akajibu, akasema, Hasha! Bwana wangu, mimi ni mwanamke mwenye roho ya huzuni, mimi sikunywa divai wala kileo ila nimeimimina roho yangu mbele za BWANA.” 1Samweli 1:10, 15
iii. Kutoa Mali Zako [ Giving Your Possessions ] :
  “ Bali utamkumbuka BWANA, Mungu  wako, maana  ndiye akupaye   nguvu za kupata utajiri; ili alifanye imara agano lake  alilowapa baba zako, kama hivi leo.” Kumbukumbu la Torati 8:18.  Pia katika  Zaburi 24:1  maandiko husema,
“Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya BWANA, Dunia na wote   wakaao ndani  yake .” Mtume Paulo naye alisema  hivi ; Au hamjui  ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe; maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.  1Wakorintho 6:19-20
Kwa maana hiyo,  msingi bora wa utoaji wa ibada kama sadaka ni NIA yako ya utoaji. Mungu haangalii jinsi unavyo jitoa sana au  kiasi kile unachokitoa mbele zake , bali ana angalia  hasa nini  NIA YAKO   juu ya kutoa na kujitoa kwako na pia  anangalia  ulichobakisha baada ya kutoa.
ü Luka 21:1- 4, Marko 12:41-44 [ utoaji wa sadaka ]
ü Wafilipi 2:4-5  [ nia ya Kristo ]
   Tuwe na nia ya Kristo  ambayo ni utumishi . Marko 10:45  .

·      Tambua kuwa wewe mwenyewe na vyote ulivyo navyo siyo mali yako; wote na vyote uvionavyo ni mali ya Roho Mtakatifu [ Mungu ], hatuna chakujivunia kuwa ni chetu. Ayubu 1:21, 1Timotheo  6:6-7;  kumbuka kuwa, hatukuja na kitu  chochote duniani hivyo tulivyonavyo sasa tumepewa na Mungu na tutawajibika kuvitolea hesabu Kwake ya matumizi ya vitu hivyo  tulipokuwa hapa duniani.
·      Wajibu wetu ni kumwabudu tu na kumtumikia Mungu kwa moyo safi na kwa nia njema-hii ndiyo ibada ya kweli.

KUMBUKA: Wote walioonesha moyo wa ibada yaani kutii na kushuka / kunyenyekea mbele za Mungu  walipokea mahitaji yao yote na haja za mioyo yao.
Kile unacho kiabudu  ndicho kinakuvaa; unakuwa vile ulivyo kwa  kutegemea yule unaye mwabudu. Zingatia kuwa, ibada ni jumla ya maisha yako; maisha yako ndiyo jumla ya ibada yako.

Kitu pekee Bwana Yesu anachokitaka na kukitafuta ndani yetu ni ile roho ya ibada ya kweli  au moyo wa utii kwa Neno lake. Hebu angalia mifano hii michache ifuatayo utaona nini kilitokea pale walipo tii Neno la Kristo;

§  Na tazama, mwanamke Mkananayo wa mipaka ile akamtokea, akampazia sauti akisema, Unirehemu, Bwana, mwana wa Daudi; binti yangu amepagawa sana na pepo. Naye akaja akamsujudia, akisema, Bwana, unisaidie. Akajibu, akisema, Si vema kukitwaa chakula cha watoto na kuwatupia mbwa. Akasema, Ndiyo, Bwana, lakini hata mbwa hula makombo yaangukayo mezani pa bwana zao. Ndipo Yesu akajibu, akamwambia mama, imani yako ni kubwa; na iwe kwako kama utakavyo. Akapona binti yake tangu saa ile.
 ( Mathayo 15:22, 25, 26, 27 na 28. Marko 7:24-30 )
o  Lengo la Yesu hapa la kumwambia mwanamke huyu kuwa ni mbwa ilikuwa nikutaka kuona kama atakasirika na kususa kwa kumdhalilisha mbele za watu. Japo kibiblia Mtu asiye mwamini Yesu ni mbwa, ila ni hatari sana hasa kwa jamii yetu kumwita mwenzako mbwa ; maana inaweza kuwa vita kali sana. Ila mama huyu haikumsumbua na matokeo yake akaukumbatia muujiza wake mara. Wengi hukimbia changamoto; kumbe hapohapo ndipo kwenye majibu yako.

§  Na hapa palikuwa na mtu , ambaye amekuwa hawezi kwa muda wa miaka thelethini na minane. Yesu alipo mwona huyu amelala, naye akajua ya kuwa amekuwa katika hali hiyo siku nyingi , akamwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapo tibuliwa, ila ninapokuja mimi , mtu mwingine hushuka mbele yangu. Yesu akamwambia , simama, jitwike godoro lako, uende. Mara yule mtu akawa mzima , akajitwika godoro lake , akaenda. Nayo ilikuwa ni siku ya sabato siku hiyo. Yohana 5:5-9.

o  Kwa haraka kama binadamu ungejiuliza na kuhoji ; hivi ina maana Yesu kweli, haoni kabisa na inaonesha  hana huruma kwa huyu mgojnwa kumbebesha godoro na ili hali hajiwezi. Hapa Bwana Yesu alikuwa anataka kuiona roho ya ibada kwa huyu mgonjwa, kitendo cha yeye tu kutii kauli ya Yesu ya kubeba godoro kili umba  na kufungulia [ activate ] uponyaji wa kipee kwenye mwili wake na kuinuka mara moja na kuanza kufanya mambo aliyokuwa hawezi kufanya hapo mwanzo.

§  Alipokwisha kusema hayo, alitema mate chini. Akampaka kipofu tope za macho, akamwambia, Nenda kanawe katika birika ya Siloamu, ( maana yake, Aliyetumwa ). Basi akaenda akanawa; akarudi anaona. Yohana 9:6-7
Katika fungu hilo hapo juu,  kitu pekee alichokuwa anakitafuta  Yesu kwa huyu kijana kipofu ni ile roho ya ibada ; utii juu ya kile alichomwambia kufanya. Mara zote miujuza yetu imeambatanishwa / imefungamanishwa  na utii wetu juu ya Neno la Mungu.  Nje ya kulitii Neno la Mungu tusitarajie kuyaona yale tumwombayo Bwana Yesu ya kitendeka maishani mwetu. Kwani utii kidogo si utii kabisa. Tunacho jifunza hapa ni kwamba, kitendo cha kijana huyu kutii kwenda kunawa bila kuhoji kuwa atakwendaje kwani haoni, kilizaa muujiza wa kurudi akiona. Haleluya! Haleluya!

§  Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simon, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki. Simoni akamjibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi yakuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa Neno lako nitazishusha nyavu. Basi, walipofanya hivyo walipata samaki wengi mno, nyavu zao zikaanza kukatika; wakawapungia mikono washirika wao waliokuwa katika chombo cha pili, waje kuwasaidia; wakaja, wakavijaza vyombo vyote viwili, hata vikataka kuzama. Simoni Petro alipoyaona hayo, alianguka magotini pa Yesu, akisema, ondoka kwangu, kwa kuwa  mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana. Yesu akamjibu akamwambia, Simoni, usiogope, tangu sasa utakuwa unavua watu. Luka 5:4-10  
·      Unaona , hapa kama Petro angekataa kutii neno la Bwana Yesu, akabaki kujivunia ujuzi wake , nguvu na akili zake  na hali  ile ya kushindwa wala asingepata wale samaki. Lakini roho ya utii / ibada ilizaa muujiza wakutisha wa kupata samaki wengi mno; na jambo la kushangaza samaki walipatikana katika bahari ileile na eneo lilelile na nyavu zilezile! Kitu kinacho takiwa ni kuzamisha na kuongeza imani na utii  kwa Neno la Yesu. Hata kwako leo inawezekana kabisa pale tu ukiinua kiwango cha ibada yako mbele za Mungu. Tatizo la  watu wengi ni kwamba hutaka Bwana afanye watakavyo wao na si kama atakavyo Mungu. Hebu tuli tii Neno la Mungu ili lizae mambo mazuri tuyatamanio maishani mwetu. Maana Neno la Mungu lilikusudiwa kutiiwa-yaani kulitendea kazi.  

”Basi Naamani, jemedari wa jeshi la mfalme wa Shamu, alikuwa mtu mkubwa mbele ya bwana wake, na mwenye kuheshimiwa, kwa sababu kwa mkono wake BWANA alikuwa amewapa Washami kushinda; tena alikuwa mtu hodari wa vita; lakini alikuwa mwenye  ukoma.”
§  Ndipo Naamani aliposikia habari za mtumishi wa Mungu Nabii Elisha akaenda ili akaombewe na kuponywa ukoma wake. Elisha kwa uongozi wa Roho wa Mungu akamwambia aende akajichovye mara saba katika mto Yordani. Lakini  Jemedari , Naamani alikataa pale alipo ambiwa kuwa akajichovye kwenye mto Yordani ; ila baada ya kushauriwa sana na watumishi wake alikubali akatii agizo la mtumishi wa Mungu , Nabii Elisha, matokeo alipona na kutakasika ukoma  wake kabisa  ; hii ni kwa sababu alionesha roho ya ibada ambayo ni utii.
“Ndipo akashuka, akajichovya mara saba katika Yordani, sawasawa na neno lake yule mtu wa Mungu; nayo nyama ya mwili wake ikarudi ikawa kama nyama ya mwili wa mtoto mchanga, akawa safi.”  2 Wafalme 5:1, 14

KUMBUKA: Huwezi kupokea muujiza au majibu ya maombi yako  mpaka tu umeonesha roho au moyo wa ibada; yaani  moyo wakushuka chini, heshima na utii mbele za BWANA YESU.

Mara zote ukisoma Mwanzo mpaka Ufunuo utaona kuwa, kila aliyemwendea Yesu akitaka uponyaji au msaada wowote ule kwake,  kwanza;  Yesu alimpa wajibu wakufanya ikiwa kama sehemu ya kuangalia moyo wa ibada , yaani kutii .



SURA YA PILI:
AINA ZA IBADA.
Kuna aina kuu  mbili [ 2 ] za ibada, ambazo ni:-
1. Ibada inayo kubalika mbele za Mungu.
2. Ibada isiyokubalika mbele za Mungu.
1. Ibada inayo kubalika mbele za Mungu.
Hii ni aina ya ibada yenye kibali mbele za Mungu, kwani imejikita kwenye misingi bora ya ibada.
·     Misingi mikuu miwili  ya ibada inayokubalika mbele za Mungu ni:

i.  Kumwabudu Mungu katika Roho;  Yohana 4:23
ii. Kumwabudu Mungu katika Kweli; Yohana 4:23


I. Kumwabudu Mungu katika roho;  Yohana 4:23
§  Hii ni ibada inayotokea ndani kwenda nje; na siyo kutokea nje kwenda ndani. Ibada hii haiangalii na wala haiamriwi au kutegemea mazingira fulani; bali  shauku ya mwabudu hapa ni huhakikisha amempa Mungu nafasi ya kwanza katika maisha yake yote kwani kwake mtu huyu , Mungu ndiye kipaumbele cha kwanza, na ndipo mambo na mahitaji yake binafsi yanafuata baadaye. “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mathayo 6:33. Pia katika kitabu cha Matendo ya Mitume maandiko yanasema;  “Lakini panapo usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za kumsifu, na wafungwa wengine wakiwasikiliza. Ghafula pakawa na tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisikika, na mara hiyo milango ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa. ” Matendo ya Mitume 16:25-26

vJe, unafikiri nini kingetokea  kama Paulo na Sila wasinge mfanyia Mungu ibada mle gerezani? Hebu jaribu kuwaza pamoja nami; kuwa,  watumishi hawa wapo kwenye maumivu makali ya kupigwa na vifungo vya kamba pamoja na njaa kali; lakini mbali na hayo yote hawakuruhusu mazingira magumu ya gerezani kuwa kikwazo  cha kumwabudu Mungu wao; kwani walijua fika kuwa Mungu wanaye mtumikia na ambaye amekuwa sababu ya wao kupata mateso makali , peke yake ndiye atakaye waponya pale tu watakapo mpa nafasi ya kwanza hata kwenye mazingira magumu. Na Mungu hakuwaacha bali alishuka ndani ya gereza na kuwatoa wote baada ya kuikubali ibada yao.

Kuna baadhi ya watu kwao ili Mungu awe Mungu kweli ni pale atakapo fanya wanayoyataka; lakini kumbuka kuwa, Mungu atabaki kuwa Mungu hata kama hakufanya au kujibu kama ulivyomwomba. Wewe endelea kumwabudu katika Roho na kweli tu naye atafanya wajibu wake.

§  Ibada hii inaongozwa na kusimamiwa na  Roho Mtakatifu mwenyewe ndani ya mwamini, ambapo milango mitano ya fahamu haina nafasi katika ibada hii; mwabudu haongozwi tena na mazingira bali yeye ndiye anayeya ongoza mazingira . Hapa ndipo roho ya mtu huungana na Roho Mtakatifu kumwabudu Mungu.

§  Kwa maana Mungu, nimwabuduye katika roho yangu katika Injili ya Mwana wake, ni shahidi wangu jinsi niwatajavyo pasipo kukoma.
o  Warumi 1:9
§  Ee nafsi yangu, umhimidi BWANA. Naam, vyote vilivyomo ndani yangu vilihimidi jina lake takatifu.
o  Zaburi 103:1
§  Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu , hutaudharau. Mstari wa 17.
o  Zaburi 51:15-17
vMwabudu huwa na nia na dhamiri safi ya kumwadhimisha Mungu wake hata kama Mungu hakufanya kama alivyotaka au alivyo omba.

KUMBUKA: Kama moyo wako hauko sawa , basi hata ibada yako haitakubalika mbele za Mungu. Na kama tulivyo ona hapo mwanzo kuwa ibada ni sadaka mbele za Mungu, hivyo basi sadaka yoyote iliyo bora lazima itoke kwa Mungu mwenyewe.
o  Mfano:
vIsaka alitoka kwa  Mungu; huyu alikuwa ni  mwana wa ahadi. Mwanzo 17:15-19 ; 21:1-5
Baada ya Mungu kumpa Ibrahim , Isaka huyo huyo tena , Mungu akamtaka Ibrahim amtoe sadaka. Mwanzo 22:1-2, 9-19

vYesu , alitoka kwa Mungu;  Isaya 7:14, Mathayo 1:21-23, Yohana 3:16 na Wafilipi 2:5-11
“Tazama, bikira atachukua mimba, naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi.”
Yesu alistahili na kufaa kwani alikuwa ni mwana wa pekee wa Mungu, lakini pamoja na hayo yote Mungu alimtoa ili awe sadaka kwa ajili ya kuukomboa ulimwengu kutoka kwenye utumwa wa dhambi na makucha ya shetani kisha kumrudishia mwanadamu ufalme / utawala alio upoteza Adamu pale bustanini Edeni.
Hivyo basi , ibada inayoongozwa na Roho Mtakatifu itakubalika mbele za Mungu kwani ni sadaka iliyo bora itokayo kwa Mungu mwenyewe; kwani Roho  Mtakatifu ni Mungu kamili kabisa.
Yohana 4:24

KUMBUKA: Bila Roho Mtakatifu  ni vigumu na wala haitawezekana kabisa kumwabudu Mungu katika roho na kweli ; bali utakuwa kimwili zaidi. Hivyo sasa tunamhitaji Roho Mtakatifu ili tuweze kutoa ibada bora na inayokubalika mbele za Mungu. “Tena msilewe kwa mvinyo,  ambamo mna ufisadi; bali mjazwe Roho. ..”Waefeso 5:18-21


II. Kumwabudu Mungu katika  kweli; Yohana 4:23
Kweli ni visivyo onekana ambavyo kimsingi  ni vya milele na milele. Jumla ya kweli yote ni Mungu na Neno lake.
ü Zaburi 119:142, 160,  2Wakorintho 4:2 , Warumi 1:18- 19, Yohana 18:37-38; 17:17-19.  Jumla ya neno lako ni kweli , Na kila hukumu ya haki yako ni ya milele.  Mfano , Mungu ni kweli, Yesu ni kweli, Roho Mtakatifu ni kweli, Neno ni Kweli.

ü 2 Yohana 1:2 ; kwa ajili ya hiyo kweli ikaayo ndani yetu, nayo itakuwa pamoja nasi hata milele.
Hii sasa ni ibada ambayo misingi yake imejengwa na kukitwa kwenye Neno la Mungu na siyo hisia na msukumo wa nje.   

Angalizo:
§  Usichanganye Kweli ya Mungu na uongo / uovu. 2Wakorintho 4:2
§  Katika maisha yako ya ibada hakikisha unabaki katika msingi wa Neno la Mungu ambayo ndiyo kweli; hata kama milango yako mitano ya fahamu inaonesha au kupingana na hali halisi bali wewe angalia kweli yaani Neno la Mungu lina sema nini. Hivyo sasa kama mwabudu halisi hakikisha kuwa umejaa Neno la Kristo kwa wingi. Wakolosai 3:16 ; kwani ujazo wake kwa wingi ndani yako kutakufanya utoe ibada ya nguvu, iliyo  hai na ya kweli baada ya kuwa umelitii na kuliishi nakukubadilisha tabia, mawazo , nia , hisia,utashi, ufahamu,akili, elimu, hekima, imani ,na mwenendo wako wa kila siku. Waebrania 4:12 -13
Matokeo ya ibada inayokubalika:
                                                   i.        Mungu Hutukuzwa.  Zaburi 50:23; Atoaye dhabihu za kushukuru, ndiye anayenitukuza. Naye autengenezaye mwenendo wake, Nitamwonesha wokovu wa Mungu.
ii. Waamini Wanasafishwa.  Zaburi 24:3-4; Ni nani atakayepanda katika mlima wa BWANA? Ni nani atakayesimama katika patakatifu pake? Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe, Asiyeinua nafsi yake kwa ubatili, wala hakuapa kwa hila.  
KUMBUKA: Ili mwamini afae kumwabudu Mungu lazima maisha yake yawe safi; hivyo tunapaswa kuishi maisha yatoba na  kujitakasa kila siku ili ibada yetu ipate kibali mbele za Mungu. 2Wakorintho7:1 –tunapaswa kujitakasa nafsi zetu kutokana na kila kinachotia unajisi mwili na roho huku tukitimiza utakatifu wetu kwa kumcha Mungu.
iii. Kanisa linajengwa na kuongezeka.
Matendo 2: 41-47; 5:28;  Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali. Na siku zote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu, wakiumega mkate nyumba kwa nyumba, na kushiriki chakula chao kwa furaha na kwa moyo mweupe. Wakimsifu Mungu, na kuwapendeza watu wote. Bwana akalizidisha kanisa kila siku kwa wale walio kuwa wakiokolewa.
Kwa hiyo, maongezeko na madhihirisho ya nguvu za Mungu pamoja na ishara na miujiza hutokea pale tu waamini watakapo inua viwango vyao vya ibada na ushirika kwa waumini wengine na kwa Mungu.

SURA YA TATU:
JINSI / NJIA  YA KUMWABUDU MUNGU KATIKA ROHO NA KWELI.
[ METHOD OF WORSHIP ].
Njia pekee ya  kumwabudu Mungu katika roho na kweli ni:-
                   i.        Kujaa Roho Mtakatifu Na Neno La Mungu;
Ni kile kitendo cha kuongozwa na Roho Mtakatifu. Ukitawaliwa na Roho na Neno utaweza kuimba Neno, kuomba Neno, kuongea Neno, kuishi Neno na kulitii Neno –yaani kulitendea kazi ,kwani maisha yako yamemjaa Mungu.
ü Waefeso 5:18; Tena msilewe kwa mvinyo, ambamo mna ufisadi ( matumizi mabaya ya mali isiyo ya kwako uliyo kabidhiwa kuwa msimamizi-wakili na Mungu ) ; bali mjazwe Roho. Tazama pia , Warumi 8:14,
ü 1Wakorintho 2:11-12; Maana ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu. Bali sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyo kirimiwa na Mungu.

                                          ii.        Kuelekeza mawazo yako yote kwa Mungu .
[ Thoughts centered to God ];
Ni ile hali ya kuweka ufahamu wako na akili zako zote juu ya Mungu. Kumtegemea Mungu kwa kila jambo. Wakolosai 3:2;  “yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi.
iii.   Kutafakari juu ya Neno la Mungu [ meditating God’s Word ];
 Haya ni maisha ya kutenga muda wa kutosha wa kusoma Neno kwa kujiuliza na kuomba katika Roho. Kama vile mwili unavyo hitaji lishe bora ili kukua , kustawi na kuimarika hali kadhalika roho ya mwabudu inahitaji lishe bora ambayo ni Neno la Mungu kila siku. Mathayo 4:4, Yoshua 1:8
ü 2Wakorintho 2:10; Lakini ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu. Zaburi 27:4- kuutafakari uzuri wa Mungu siku zote hekaluni mwake. Tazama pia Luka 10: 38-42- kaa chini ya miguu ya Yesu ili umsikilize na kusikia anasema nini juu ya maisha yako.

KUMBUKA:  Ni katika kutafakari tunapo pata ufunuo wa Neno la Mungu. Na ili tupate ufunuo safi juu ya Neno la Mungu tunahitaji kuwa na ushirika wa karibu na Roho Mtakatifu. 2 Wakorintho 13:14, 1Wakorintho 2:10-13.


SURA YA NNE:
SURA , PICHA AU MWONEKANO WA IBADA INAYO KUBALIKA.
                     Sura ni ule mwonekano wa kitu au jambo fulani.
Sura ya ibada inayokubalika kwa  Mungu ni manukato au harufu nzuri mbele zake. Kutoka 30:34-38; 37:29, Zaburi 45:8, Ezekieli 27:22, Yeremia 6:20 na Wimbo ulio bora 4:14
BWANA, akamwambia Musa, Jitwalie manukato mazuri, yaani natafi, shekelethi, na kelbena; viungo vya manukato mazuri pamoja na ubani safi; vitu hivyo vyote viwe ni vya kipimo kimoja.
Yohana 12:3-8; Basi Mariam akatwaa ratli ya marhamu ya nardo safi yenye thamani nyingi, akampaka Yesu miguu, akamfuta miguu kwa nywele zake. Nayo nyumba pia ikajaa harufu ya marhamu.
2Wakorintho2:14-16; Ila Mungu ashukuriwe, anayetushangiliza daima katika Kristo, na kuidhihirisha harufu ya kumjua yeye kila


mahali kwa kazi yetu. Kwa maana sisi tu manukato ya Kristo, mbele za Mungu, katika wao wanaookolewa, na katika  wao wanaopotea. Katika hao wa pili harufu ya mauti iletayo mauti; katika hao wa kwanza harufu ya uzima iletayo uzima. Naye ni nani atoshaye kwa mambo hayo?



KUMBUKA: Ibada inayokubalika huwa kama manukato mazuri yanayo mfanya Mungu ajisikie vizuri; hivyo humfanya ashuke ili  kutuhudumia watoto Wake. Ili maisha yetu yawe ya mvuto na harufu nzuri ya kupendeza mbele ya Mungu inatupasa kujitakasa kila siku maadam tunaishi. 1Yohana 3:3; “Na kila mwenye matumaini haya katika Yeye hujitakasa, kama Yeye alivyo Mtakatifu.
Kwa hiyo, Sifa kuu ya Mungu ni Utakatifu / usafi, kama vile mtu asivyopenda kukaa na mtu mchafu, anayetoa harufu chafu kama vile kikwapa , miguu, kinywa, n.k hivyo si  zaidi sana kwa Mungu wetu? Yeye ni Mtakatifu hivyo na sisi imetupasa kuishi maisha Matakatifu yasiyo na michanganyo / ila / mawaa au lawama  mbele zake na mbele za wanadamu. 1 P eter 1:16; Maana imeandikwa mtakuwa watakatifu kwa kuwa Mimi ni Mtakatifu.

Kwa msingi huo, maisha yetu yakiwa safi chochote tukifanyacho mbele za Mungu kitakuwa ni kama manukato mazuri, hata unapo omba , maombi yako yatakuwa manukato mazuri mbele ya kiti cha enzi, yaani Mungu atakuwa anajisikia na kufurahia kwa kile ukifanyacho. Tazama, Ufunuo 5:8; Hata alipo kitwaa kile kitabu, hao wenye uhai wanne na wale wazee ishirini na wanne wakaanguka mbele za mwana-kondoo, kila mmoja wao ana kinubi, na vitasa vya dhahabu vilivyo jaa manukato, amabyo ni maombi ya watakatifu.








SURA YA TANO
SIFA ZA JUMLA ZA MWABUDU.
Mtoa ibada ya kweli au mwabudu halisi [ the true worshiper ] lazima awe na sifa zifuatazo:-
i.  Awe mtu aliyejaa Imani:
Imani ni kuishi maisha ya kumtegemea Mungu na Neno lake. Hii humanisha kwamba ,kile alicho sema Mungu kwenye Neno lake ni lazima aamini kuwa ni kweli na kwamba atafanya kama alivyo sema. Maana mwenye haki anaishi kwa imani, na pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu kwenye maisha yetu. Kama humwamini Mungu hufai kumwabudu. Ni vigumu kuwaaminisha watu kwa  Mungu usiye mwamini. Wapo watu wanao amini kuwa Mungu anaweza kufanya mambo yote ila siyo kwao bali kwa wengine. Imani ndiyo mikono ya kupokelea majibu yetu. Matendo 6:5-6, Waebrania11:1,6; Warumi 1:17 
ii.  Awe na maisha matakatifu:  
       1 P eter 1:16; Maana imeandikwa mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu. Wakorintho 3:16-17; Hamjui kuwa ninyi mmekuwa  hekalu la Mungu, na ya kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu? Kama mtu akiliharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ndilo ninyi. Mwabudu anapaswa kuwa kioo au kielelezo , maisha yake yawe na ushuhuda mzuri wa maisha safi yasiyo natuhuma wala lawama. Kwani , Mungu anapendezwa na watakatifu walioko duniani maana ndiyo walio bora. Zaburi 16:3.
iii.  Awe amejaa upendo:
 Haya ni maisha ya  kutoa na kujitoa kwa ajili Mungu kwanza pili kujitoa kwa ajili ya wengine. Ukipenda kitu utakifanya kwa moyo wa furaha bila kuhesabu gharama-yaani bila kutazamia malipo kutoka kwa watu. Ukimpenda Mungu utajitoa kwa ajili ya kumwabudu na kutumiwa na wengine kwa kadri watakavyo kwani upo kwa ajili ya kulitumikia kusudi la Mungu. Yohana15:13, hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.  Tazama pia , Yohana 3:16, 1Yohana 3:16.
iv.  Awe amejaa Neno la Mungu:
 Biblia inatusihi sana juu ya kujaa Neno la Mungu kwa wingi na katika hekima yote, Wakolosai 3:16. Yesu akajibu, akamwambia, Mtu  akinipenda atalishika Neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake.
 Yohana 14:23. Ukijaa neno , utasema neno, utaimba neno, utaomba neno, utaliishi Neno, jambo ambalo litakufanya kushinda mazingira yote yakutenda dhambi maishani. Zaburi 119:9-12.
v. Awe amejaa Roho Mtakatifu:
Matendo 6:5-6, Stefano alikuwa ni mtu aliyekuwa amejaa Roho Mtakatifu. Ushirika mzuri na Roho Mtakatifu utakuwezesha kumfanyia BWANA ibada ya kweli. Ukikosa ushirika na Roho Mtakatifu itakuwa ni vigumu sana kuwaongoza watu wengine kumtolea  Mungu ibada bora yenye kibali kwake. 2Wakorintho 13:14.  Kwani hutaweza na nivigumu  kuwapeleka watu mahali wewe hujafika. Ili watu wakuelewe na wafuate unachokisema ni pale utakapo kiishi unachokisema. Hakikisha maisha yako yawe yameathiriwa na Roho Mtakatifu. Waefeso 5:18- tulewe Roho Mtakatifu.
vi.  Awe mtu wa sala / maombi:
Tunaomba ilikupata msaada wa Mungu katika yale tunayo taka kuyafanya. Lengo kuu la maombi ni kupata mwongozo sahihi wa Mungu. Vile unataka jambo liwe unaliumba au unalitengeneza kwenye maombi. Mungu ametuagiza kuomba kwani ndiyo moja ya njia ya kuwasiliana naye. Anesema katika; Yeremia 33:3; “Niite, nami nitakuitikia nami nitakuonyesha mambo makubwa, magumu usiyo yajua. “  Pia Zaburi 105:4 ; anasema mtafuteni BWANA pamoja na nguvu zake. Swali la kujiuliza namwitaje na kumtafutaje Mungu? Jibu ni kwa njia ya maombi/ kuzungumza naye. Hivyo mpendwa fanya maombi ngazi ya kubisha [ maombi ya ngazi ya patakatifu papatakatifu] ya kuomba katika roho. Mathayo 7:7;
·      Kuomba [ ask ]- mwilini ; maombi ngazi ya ua wa nje.
Maombi yanayo tawaliwa na milango mitano ya fahamu ,haya ni maombi baridi. Kiwango hiki hakina matokeo wala madhara kwa adui. Hapa ukiuliza unajibiwa tu. Mfano unaitwa nani?  Amani.  Hii haitakusaidia sana.

·      Kutafuta [seek ]- nafsi; maombi ngazi ya patakatifu;
Ni maombi yanayo tawaliwa na hisia na uzoefu / mazoea , akili na Neno kidogo; ni maombi ya uvuguvugu. Kiwango hiki cha maombi pia hakina matokeo mazuri na Mungu hukaa pembeni- utatapikwa na Mungu; mpaka umalize ujanja wote. Hapa mtu akitafuta  atapata anachokitafuta kwa bidii yake wala Mungu hahusiki na wewe.
·      Kubisha [ knock ]-roho; maombi ya ngazi ya patakatifu papatakatifu;
 Ni maombi yanayo tawaliwa na Roho Mtakatifu. Haya ni maombi ya moto mkali. Kiwango hiki cha maombi ni hatari kwa adui na wala hawezi kukusogelea na matokeo yake ni makuu sana. Hapa kila anaye bisha lazima afunguliwe tu; na ukisha funguliwa mlango nikuingia na kujichukulia unachotaka mbele za Mungu wako. Haya ni maombi ya maarifa na ufahamu wa juu katika ulimwengu wa roho. Hivyo tunapaswa kuomba siku zote wala tusizimie na kukata tamaa; Luka 18:1-8
vii.  Awe mnyenyekevu:
Mwabudu halisi na wakweli lazima  awe mnyenyekevu, kwani anajua wazi kuwa karama, vipawa na huduma  alivyo navyo si kwa ajili yake ni kwa ajili ya wengine. Na wala siyo vyake amepewa tu bure nay eye huwa tu ni wakili. Hivyo roho ya kiburi haitatajwa kwake kamwe ; kwani Mungu huwapinga wenye kiburi bali huwapa wanyenyekevu neema. Ni kweli mtu akifanya vizuri watu watamsifia lakini wewe usizibinafsishe hizo sifa bali mrudishie Mungu mwenyewe.
ü 1Petro 5:5-6; Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake, tazama pia ; Yakobo 4:6-7, Mithali 3:34, Ayubu 22:29
KUMBUKA: Mtu anapo kusifia kwa kufundisha vizuri , kuhubiri vizuri, kuimba vizuri , n.k jua kuwa kinacho sifiwa siyo wewe bali ni kile kipawa au ile karama na huduma iliyo ndani yako ambapo kimsingi imetoka kwa Mungu mwenyewe.

vMsingi Mkuu wa ibada inayokubalika mbele za  Mungu ni USAFI / UTAKATIFU. Katika Zaburi 24:3-4; maandiko husema, “ Ni nani atakaye panda katika mlima wa BWANA? Ni nani atakayesimama  katika patakatifu pake? Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe, Asiyeiinua nafsi yake kwa ubatili, Wala hakuapa kwa hila.

Maandalizi ya ibada inayokubalika mbele za Mungu.
Ni jambo jema kujiandaa unapo taka kwenda mbele za Mungu. Kuna baadhi ya watu waliokwenda mbele za Mungu kumfanyia ibada wakiwa wazima wakarudi wakiwa wagonjwa, wengine walienda wakiwa hai wakarudi maiti. Kwa nini? Kwa sababu Mungu siyo Mungu wa mazoea ; ni Mungu wa kanuni na taratibu. Walawi 16:1-7
Hivyo, sasa ni vizuri sana kusafisha mazingira yako yakukutania na Mungu wako kwa kufanya maombi ya rehema na utakaso mbele za Mungu kwa lengo la kupatana na Mungu ili tu asione kitu kichafu kisichofaa kwako akageuka na kukuacha; Kumbukumbu la Torati 23:14; Waebrania 4:16; 10: 19-22, Mithali 3:3-4, 1Yohana 3:21 na Yakobo 4:7.
Tazama pia Yakobo 3:2.    Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”   Mungu  anaposhuka anakuja kuhukumu vyote vilivyo kinyume na ufalme wake. Hivyo ikitokea akakukuta umeharibu na kuchafua ushirika pamoja naye, atakuharibu. Tazama jinsi Mtume Paulo anavyo likazia jambo hili katika; 1Wakorintho 3:16-17; “Hamjui kuwa ninyi mmekuwa  hekalu la Mungu, na ya kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu? Kama mtu akiliharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ndilo ninyi.”

Kumbe saa tunaona kwamba  msingi mkuu wa maandalizi ya ibada yenye maana na kukubalika  mbele za Mungu ni mazoezi ya toba, rehema na utakaso  katika maisha yetu ya kila  siku, yaani usafi wa roho. 1Wathesalonike 5:23; Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi roho zenu na nafsi zenu na miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.







 

SURA YA SITA
IBADA ISIYO KUBALIKA MBELE ZA MUNGU.
Ni jambo la kusikitisha, kuogofya na kuumiza sana; la mtu kwenda mbele za Mungu kumwabudu kisha ibada yake  ikakataliwa. Kumbuka kuwa ibada ni sadaka na kama sadaka basi,  ikitokea sadaka yako imekataliwa hii ina maanisha kwamba na wewe mwenyewe umekataliwa vilevile. Tazama Mwanzo 4:1-15 utakuta wana wa Adamu,  Kaini na Habili walitokeza mbele za BWANA ili kumfanyia ibada ya kumtolea sadaka. Tunaona sadaka ya mmoja aliye mdogo [ Habili ]  ina kubalika na kupata kibali kwa Mungu ila ya mwingine mkubwa [ Kaini ] haikupata kibali yaani haikukubalika mbele za Bwana. Mwanzo 4:3-5   inasema  kuwa ; Ikawa hatimaye, Kaini akaleta mazao ya ardhi, sadaka kwa BWANA. Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizo nona za wanyama. BWANA akamtakabali Habili na sadaka yake; bali Kaini hakumtakabali, wala sadaka yake. Kaini akaghadhibika sana, uso wake ukakunjamana.
Nini hutokea sasa kwa mwamini kama  ibada yake imekataliwa?
Vifuatavyo ni viashiria kuwa mtu huyu ibada yake mbele za Mungu haina kibali; ni kama anapoteza wakati tu kujihudhurisha kwenye makusanyiko ya watu wa Mungu. Na kundi hili ndilo kubwa sana. Viashiria hivi ni:-
                      I.        Anatawaliwa na roho ya chuki [ hatred spirit ]
                    II.        ana roho ya wivu [jelous spirit ]
                  III.        amejaa roho ya kuhukumu na kukosoakosoa wengine [ judgementalism spirit ]
                  IV.        ni mtu aliye na roho ya uchungu [ bitterness spirit ]
                    V.        anatawaliwa na roho ya kiburi [ eaglism spirit ]
                  VI.        mtu wa kujali mipango yake kwanza kuliko mipango ya ufalme wa Mungu .Kitu ibada, Neno la Mungu kwake ni ziada.
                VII.        Mtu mwenye  roho ya kutokuonyeka
              VIII.        ametawaliwa na roho ya uchoyo na ubahili hata kwa Mungu.
                  IX.        amejaa roho ya ubinafsi [ selfishness ]
                    X.        hujiona kuwa yeye ni bora kuliko wengine.
                  XI.        anafanya mambo ya Mungu kwa mazoea [ familiar spirit ]- Waamuzi 16:20-22
                XII.        ana roho ya dharau. 1Samweli 2:30
              XIII.        ni mwizi / kibaka wa mafungu ya kumi [ robber ] Malaki 3:8-11
              XIV.        hana moyo au roho ya shukurani- Mithali 16:18
                XV.        amejaa roho ya manung’uniko na lawama. Hesabu 11:4-11; 14:1-12
              XVI.        hudharau na haheshimu uongozi na viongozi; haongozeki. Hesabu 16:1-35 habari za Kora kuinuka kinyume cha Musa; na matokeo yake.
            XVII.        huongelea vibaya kanisa lake na watumishi.
          XVIII.        hutoa sadaka vilema akidhani anamkomoa mchungaji. Malaki 1:6-14;
              XIX.        ana roho ya kususa kufanya huduma akidhani ana wakomoa viongozi.
                XX.        anaishi maisha machafu yasiyo na ushuhuda mzuri mbele ya jamii yake-maisha yake humtukanisha Kristo na kuwazuia watu wasimwamini Bwana Yesu.
              XXI.        hana roho ya toba hata kidogo, dhamiri yake imetiwa ganzi.
            XXII.        mtu wakufuatilia na kujihusisha sana na mambo ya watu kuliko Neno la Mungu.
          XXIII.        haongozwi tena na Roho Mtakatifu bali huongozwa na milango mitano ya fahamu, yaani mwili.
          XXIV.        mchongezi, wazushi na mgomvi
            XXV.        ana roho ya unafiki [ hypocrisy ]
              Kutoka 4:1-15, Malaki 3:8-11; 2:1-4, Zekaria 5:1-4


Mifano ya ibada zisizo kubalika mbele za Mungu.

Zifuatazo ni baadhi tu ya ibada zisizo kubalika mbele za Mungu:-
a) Ibada itolewayo kwa miungu [ the worship of false gods];
miungu ni vitu vinavyo chukua nafasi ya Mungu.  Vitu hivi vyaweza kuwa fedha, mali, wazazi, kazi  na n.k ; hivi ni  vitu vya dunia [ earthly materials ]  na sanamu za mfano wa   vitu vya mbinguni [ heavenly things ] ambavyo humpelekea mtu  kumfanya Mungu kuwa wa baadaye kabisa. Bwana  ni Mungu mwenye wivu.  Kutoka 34:14;  “maana hutamwabudu mungu mwingine, kwa kuwa BWANA, ambaye jina lake ni mwenye wivu, ni Mungu mwenye wivu. “  Tazama pia- Ayubu 31:24-28, Yoshua 24:19- 20, -ukimwacha BWANA na kuitumikia miungu migeni, ndipo atageuka na kuwatenda mabaya na kuwaangamiza baada yakuwatendea mema. Kumbukumbu la Torati 4:14-19 na Marko 4:19

b)Ibada itolewayo kwa Mungu wa kweli katika njia au mfumo mbaya.
[ the worship of the true God in a wrong form.];
Tazama Kutoka 32:1-28, utaona Haruni na wana wa Israeli wameamua kuyeyusha ndama ili kumwabudu baada ya kuona Musa amekawia kurudi kutoka mlimani. Mungu hatapokea ibada itolewayo kwake kwa mfumo mbaya; hapa ni sawa na mtu anaye asi maagizo au neno la Bwana.

c)  Ibada itolewayo kwa Mungu wa kweli kwa namna au kwa mtazamo wa mtu apendavyo yeye. [ the worship of true God in self – styled manners ];

Hii ni roho ya mazoea ya mtu kujiendea hovyo hovyo au kukosa utaratibu nyumbani mwa Mungu.  Usiende mbele za Mungu kwa mazoea ukifikiri ni Mungu wakumzoelea; usimkariri Mungu, kama jana alitumia kitu fulani basi au alipitia njia fulani leo anaweza kuja na kitu kingine kabisa. Kama jana alikupa ufunuo fulani usitumie ufunuo wa jana leo mwamini Mungu kwa kiwango kingine; usigeuze ufunuo aliokupa jana au mwaka jana na kuufanya fundisho leo , utakuwa unakosea sana. Jiulize hicho unachokifanya leo umeambiwa na nani au isije ukawa unakariri na kutembea juu ya mafunuo na shuda za watu; kama unafanya hivyo utakuwa unawalisha watu viporo na matango mwitu. Hivyo hakikisha kile unacho kifanya au kukisema, kukiimba na kukifundisha chanzo chake au asili yake iwe ni Mungu mwenyewe. Leo utashangaa kabisa hata mtoto aliyezaliwa leo kiroho anashangaa; utakuta watumishi wengi wamegeuza ufunuo kuwa fundisho, elewa kuwa ufunuo upo ila tatizo kuugeuza ufunuo kuwa fundisho la imani  na mtindo wa Mungu kwa watu wake. Mfano matumizi ya chumvi, maji, mafuta, mchanga, kitambaa, sabuni, udongo n.k, kwakuwa tu kuna siku ulipewa ufunuo kutumia kitu fulani kwa ajili ya mtu fulani kwa wakati fulani, sasa mtumishi anageuza kuwa ndiyo mtindo na fundisho la kuwajenga watu. Huku ni kulinajisi kanisa na kuwadumaza waamini kutokulitegemea Neno la Mungu ambalo ndilo ufunuo pekee imara na endelevu.

 KUMBUKA: Mungu habadiliki wala Neno lake; bali njia za utendaji kazi wake huweza kubadilika.  Rejea katika huduma ya Yesu  wakati wa utumishi wake, alikuwa na njia mbalimbali za uponyaji: Mfano; siku moja alitema mate na kutengeneza matope kisha akampaka  kipofu machoni na kumwagiza aende kunawa kwenye birika la siloamu- Yohana 9:1-7, Yesu anaweka mikono juu ya kipofu Marko 8:22-25, mwanamke anagusa vazi la Yesu  na kuponywa ugonjwa wake- Marko 6:56,  Akawaagiza wakoma kumi kwenda kujionesha kwa makuhani ili watakasike na wakiwa njiani wote kumi walitakasika- Luka 17:12…,   Akamwamuru aliye pooza miaka 38 kubeba godoro lake mara akawa mzima- Yohana 5:8-9, Yesu analigusa jeneza  na kijana aliye kuwa amekufa akawa hai– Luka 7:14, hapa Yesu anamwamuru Lazaro aliyekuwa amekufa kutoka kaburini ,  mara akatoka akiwa hai- Yohana 11:43, Yesu analituma Neno tu na kumponya mtumishi wa afisa mmoja - Yohana 4:50, wagonjwa wanapona kwa kupitiwa na kivuli cha Petro- Matendo 5:15-16, n.k. Acha kumzoelea Mungu kabisa.  Roho ya mazoea ilimgharimu sana Samsoni, hata ikapelekea kung’olewa macho, kufungwa minyororo, kutupwa gerezani na kufanyishwa kazi ngumu za kusaga ngano.  Waamuzi 16:20-21; Kisha akasema, Samsoni, Wafilisti wanakuja. Akaamka katika usingizi wake, akasema, Nitakwenda nje kama siku nyingine, na kujinyosha. Lakini hakujua kuwa BWANA amemwacha. Wafilisti wakamkamata, wakamng’oa macho; wakatelemka naye mpaka Gaza, wakamfunga kwa vifungo vya shaba; naye alikuwa akisaga ngano katika gereza. Kwa hiyo  haya ndiyo madhara ya roho ya mazoea, kung’olewa macho, kuwekwa kifungoni na kutumikishwa kwa kazi ngumu na adui kama ilivyokuwa kwa kamanda Samsoni. Na katika Matendo ya Mitume 5:1-11; tunaona habari  ya  Anania na Safira mkewe waliokufa mbele za BWANA machoni pa waamini wote kwenye ibada aliyokuwa akihudumu Mtume Petro. Wanandoa  hawa walikufa kwa  siku moja  baada ya kuongea uongo madhabahuni kwa Mungu. Waliahidi kuuza kiwanja chao na kwamba wataleta thamani yote ya fedha ya kiwanja kanisani, lakini  baada ya kuuza wakazuia sehemu ya mali kwa siri; lakini  kwa uongozi wa Roho Mtakatifu Petro akafunuliwa uovu wao. Walipo ulizwa kwa lengo la kutengeneza na Bwana,  walizidi kukataa kuwa hicho ndicho kiasi chote cha pesa. Mara tunaona mzee Anania anapiga mweleka na kufa palepale na vijana wakaenda kumzika; baada ya masaa matatu mke wa marehemu akaingia na yeye ibadani kwanza amechelewa sana, pili wamezuia sehemu ya pesa ya Mungu [ wameiba ] na tatu uongo kwani hata alipo ulizwa kuwa kiwanja waliuza kwa pesa ambayo mme wake aliipeleka; mama huyu bila aibu wala uoga  akakubali; hata pale alipo ambiwa mume wako amekufa kwa uongo huohuo na kuonyeshwa miguu ya vijana waliokwenda kumzika hata hivyo hakutubu. Ghafla naye akaporomoka chini na kufa palepale na vijana wakaenda kumzika; huku ibada ikiendelea kama kawaida na Petro akishusha kifungu kimoja baada ya kingine. Maana yake ni nini;  kufa kwako kiroho au hata kimwili kwa uovu wako usiyotubiwa  haitamzuia Mungu  kuendelea kuwahudumia watoto wake. Hivyo angalia sana mapito / njia zako mbele za Mungu, kwani Yeye si wakumzoelea.

Katika  Walawi 10:1-20; watoto wa Haruni wanakufa mbele za BWANA kwa sababu ya mazoea- waliota moto wa kigeni mbele za BWANA ambao yeye Mungu hakuwaagiza. Akawaua  wote. Pia  katika 1Samweli 13:8-14; hapa tunaona mfalme Sauli anaingilia majukumu yasiyo mhusu ya kikuhani; matokeo yake ufalme wake haukudumu. Usiingilie majukumu yasiyo kuhusu fanya yaliyo yako. Ijue mipaka ya utumishi wako ili kuepusha ajali nyumbani mwa Mungu. Ukitazama pia katikati kitabu cha 1Wafalme 13:1-6; utaona kwamba,    Mfalme Yeroboamu alikauka mkono baada ya kufukiza uvumba madhabahuni kinyume cha taratibu.

Katika 2Nyakati 26:16-21; hizi ni habari za mfalme  Uzia aliye acha nafasi yake ya utawala na kuingilia kazi za kuhani za kufukiza uvumba, makuhani walimkataza lakini alikataa ndipo Mungu alipo amua kumpiga kwa ukoma kwenye paji la uso mpaka akafa na huo ukoma.

Ukisoma  2Samweli 6:1-9; utaona hapa Uza, anakufa mbele za BWANA kwa kosa la kulinyoshea mkono sanduku la Agano akitaka kulizuia ili lisianguke.

 KUMBUKA : Mungu ni Mungu wa kanuni.
Mathayo 15:1-9; 23:23-28; utaona maisha ya Mafarisayo na Waandishi yalikuwa ya kinafiki na yakuigiza mbele za Mungu. Walimheshimu Mungu kwa midomo yao lakini mioyo yao ilikuwa mbali na Mungu. Na ibada yao ilikuwa bure mbele za Mungu. Pia hata utoaji wao wa zaka, maombi na sadaka ulikuwa mbaya mbele za Mungu. Walikuwa wanaonekana wasafi nje lakini ndani wachafu. Tafadhali safisha ndani mwako yaani moyo wako ili ufae kumtolea Yesu ibada yenye kibali.
d )  Ibada itolewayo kwa Mungu wa kweli katika Nia mbaya.
[ the true worship of the true God with a wrong attitude ]
·     Nia ni namna mtu anavyofikiria au mtu anavyohisi au anavyo ona kuhusu mtu mwingine. Nia ni moja ya vitu vilivyo ndani ya nafsi ya mtu.
ü Warumi 12:2; Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.
Tazama mfano wa mtu aliye vurugwa nafsi yake hasa chumba cha nia, mara zote maisha yake ya ibada hayako vizuri ibada au sadaka zake huwa vipofu na kilema mbele za Mungu.  Malaki 1:6-14; mstari wa 8- Tena mtoapo sadaka aliye kipofu, si vibaya? Na mtoapo sadaka walio vilema na wagonjwa, si vibaya? Haya! Mtolee liwali wako; je! Atakuwa radhi nawe? Au atakukubali nafsi yako? Asema BWANA wa majeshi. Mungu amepiga marufuku kumpelekea matoleo au sadaka za ubatili.. Isaya 1: 11-20. Mstari wa 13

KUMBUKA: Kama tukiabudu hali mioyo na hisia zetu haziko sawa au haziko sahihi hiyo ibada haitakubaliwa na Mungu.

Na kitu pekee atakacho kifanya Mungu kwa watu wanao abudu kwa nia mbaya, anasema katika; Malaki 2:3; Angalieni, nitaikemea mbegu kwa ajili yenu, nami nitapaka nyuso zenu mavi, naam, mavi ya sadaka zenu; nanyi mtaondolewa pamoja nayo. Maana yake hawataziona Baraka za Mungu katika kile wakifanyacho na pia atawaondolea kibali.

vKiwango chako cha ibada ndicho kitakacho amua hatima yako; upo vile ulivyo kwa sababu ya kiwango chako cha ibada mbele za Mungu.

vMatatizo na changamoto nyingi kwenye maisha ya waamini wengi yanasababishwa na kuwa na kiwango kidogo cha ibada yaani kukosa roho ya utii juu ya yale tupaswayo kuyafanya kwa sababu ya roho ya mazoea. Hebu chukulia mfano huu rahisi kabisa wa wanandoa na mfano wa wazazi na watoto; unafikiri nini kitatokea mke atakapo mtii mume wake? Bila shaka mume ata mpenda sana mke wake na atatamani awe anamwona kila wakati. Waefeso 5:22-29, Wakolosai 3:18-19, Mithali 8:17 Mungu anawapenda wanao mpenda…. Na nini unadhani kitatokea watoto wakiwaheshimu na kuwatii wazazi wao? Bila shaka chochote kile watoto hawa watakacho kihitaji kutoka kwa wazazi wao, watafanyiwa.  Pia kinyume chake ikitokea mke hamtii mume wake na wala watoto hawawaheshimu wazazi wao tena; nina hakika mahusiano katika  maisha yao yatakuwa magumu sana.  Ndivyo ilivyo katika ufalme wa Mungu kwamaba  ili tupate kuyala mema ya nchi inatupasa kuyatii maagizo ya Neno la Mungu. Tazama,  Isaya 1:19-20; Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi. Bali kama mkikataa na kuasi mtaangamizwa kwa upanga; maana kinywa cha BWANA kimenena haya. Usisahau ibada ni utii.

vPia nimekuja kungudua kuwa hata vijana wengi wanapata changamoto kubwa katika mahusiano  yao kujua nani ndiye jibu sahihi kwa ajili yake kutoka kwa BWANA. Utakuta kijana maisha yake ya ibada niya ujanjaujanja halafu anategemea Mungu ampe mke au mume mwenye busara, kitu ambacho hakiwezekani kabisa; Mungu anacho kifanya anakuacha upuyange, yaani ujiendee mwenyewe ukaumie ili ujifunze kutokana na makosa. Kama unataka vya Mungu lazima vigezo na masharti vizingatiwe; kwani Mungu ni Mungu wa utaratibu.

vTuliokolewa na kumbolewa kisha tuka hamishwa kutoka kwenye ufalme wa giza na kuingizwa kwenye ufalme wa nuru ili tuweze kumwabudu na kumtumikia Mungu wetu kwa nguvu zetu, kwa akili zetu, kwa roho zetu na kwa  mali zetu. Kutoka3:12;  10:24-29.



SURA YA SABA
TOFAUTI KATI YA IBADA NA HUDUMA.
Ipo tofauti kubwa sana kati ya Ibada [worship ] na Huduma [ ministry ] ; kwa kifupi ni kwamba:-
·     Ibada kikawaida hutoka chini [ kwetu ] kwenda juu kwa Mungu kwa nguvu za Roho Mtakatifu kupitia jina la Yesu, ambapo; Huduma ni ile inayotoka juu kwa Mungu kuja chini [ kwetu ] kwa njia ya Yesu na kwa nguvu za Roho Mtakatifu kwa mfumo wa karama za rohoni.
ü 1 Wakorintho 12:1-11.
“Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yuleyule. Tena pana tofauti za huduma, na Bwana ni Yeye Yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni Yule Yule azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana.” 1Wakorintho 12:4-7 

KUMBUKA: Mungu hushushuka kuhudumu kati na ndani yetu na kukutana na mahitaji yetu pale tu anapokuwa ameipokea ibada yetu, yaani akiwa amefurahishwa na ibada yetu.

v   Tatizo na changamoto kubwa ya kanisa la leo , wakristo wengi tupo kihuduma zaidi na siyo kiibada; waamini walio kihuduma tunaweza kuwafananisha leo na kizazi cha Martha ndugu yake na Mariamu, watu wenye shughuli na utumishi mwingi kuliko kuabudu. Jambo pekee la kujifunza kwa Martha ni kuwa; anawakilisha watu walio kihuduma zaidi kuliko ibada. Na jambo pekee lakujifunza kwa Mariamu ni kuwa ; yeye anawakilisha kizazi cha waabuduo halisi ,yaani kundi la waamini walio jidhabihu au waliyotoa muda, mali na maisha yao kuwa sadaka au ibada iliyo hai kwa Bwana Yesu.  Tazama kile Yesu anachokisema kwa hawa ndugu pale alipo watembelea nyumbani kwao; kila mmoja alimpa alama zake:

ü Luka 10:38-42; Ikawa katika kuenenda kwao aliingia katika kijiji kimoja; mwanamke mmoja jina lake Martha akamkaribisha nyumbani kwake. Naye alikuwa na umbu lake aitwaye Mariamu, aliyeketi miguuni pake Yesu, akasikiliza maneno yake. Lakini Martha alikuwa akihangaika kwa utumishi mwingi; akamwendea, akasema, Bwana, huoni vibaya hivyo ndugu yangu alivyoniacha nitumike peke yangu? Basi mwambie anisaidie. Bwana akamjibu akamwambia, Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amechagua fungu jema, ambalo hataondolewa. Soma pia,  Zaburi 27:4; Neno moja nimelitaka kwa BWANA, Nalo ndilo nitakalo litafuta, Nikae nyumbani mwa BWANA siku zote za maisha yangu niutazame uzuri wa BWANA, Na kuutafakari hekaluni mwake.

Kwa hiyo fanya jambo au kitu chochote kitakacho mfanya Mungu ajisikie vizuri na kushuka kuhudumu, maana sahau kupokea kitu chema kutoka kwa Bwana kama ibada yako haijamfurahisha. Tangu kale Mungu alikuwa akishuka kuhudumu yaani kuchukua au kupokea sadaka mara tu yakupendezwa na harufu nzuri ya  sadaka au dhabihu hiyo. Mwanzo 4:4-5.

Nikupe ushauri leo; hebu tafuta kitu ambacho utakifanya katika ufalme wake / nyumbani mwa Mungu ambacho kitamfanya Mungu huko aliko ajisikie vizuri na kumfanya achilie majibu ya haja ya moyo wako na kukutendea mambo makuu ya kuushangaza ulimwengu.  



§  Uishi milele katika uwepo wa BWANA. 2Wakorintho 13:14.

 TOLEO LA PILI  ( c ) March, 2017.



1 comment: